Latest Stories

Recently Comments


Advertisement

Advertisement
TIGO PATA PATA

News

News

Chanzo cha Habari: Gazeti la Mwananchi
MWASISI wa Chadema na Mwanasheria mkongwe nchini Bob Makani, amefariki dunia usiku katika hospitali ya Aga khan, jijini Dar es Salaam.

Habari zilizopatikana na kuthibitishwa na Naibu Katibu Mkuu wa Chadema, Zitto Kabwe, Makani alizidiwa ghafla saa 3: 00 usiku wa kuamkia leo na kukimbizwa katika Hospitali ya Aga Khan ambako alifariki dunia saa 4.15 usiku.

“Amekuwa anaumwa muda mrefu, mara kadhaa akipelekwa hospitali na baada ya muda anaruhusiwa, lakini hii ya sasa alikua nyumbani akazidiwa ghafla wakampeleka hospitali na ilipofika saa 4.15 wakasema amefariki,” alisema Zitto.

Zitto alisema kuwa, suala la wapi utakapozikwa Makani ambaye ni Katibu Mkuu wa Kwanza na Mwenyekiti wa pili wa Chadema, litajulikana baada ya kujadiliana na familia ya marehemu.

“Suala la wapi atazikwa kama ni Shinyanga ama Dar es Salaam, litajulikana baada ya kuzungumza na familia yake, kwa sasa tunashughulika kwanza na kuhifadhi mwili wa mzee wetu,” alisema Zitto.
Zitto alisema msiba wa utakuwa nyumbani kwa marehemu eneo la Mbezi Beach, jijini Dar es Salaam.

Kwa siku za hizi karibuni afya yake imekuwa ikizorota na kumfanya kuripotiwa kuanguka mara kwa mara alipokuwa akifanya shughuli zake.

Januari 17 mwaka huu katika msiba wa aliyekuwa Mbunge wa Viti Maalum wa Chadema Regia Mtema, Makani alianguka muda mfupi baada ya kuuaga mwili wa marehemu.

 Baada ya tukio hilo, alibebwa na kupelekwa pembeni ambako alipepewa kwa takriban dakika tano kisha kurejea katika hali yake ya kawaida na kurudi kwenye kiti chake

Alikuwa Katibu Makuu wa kwanza wa Chadema kati ya mwaka 1993 hadi 1998, alikuwa Mwenyekiti wa chama hicho kuanzia mwaka 1998 hadi 2004 na amegombea ubunge wa Jimbo la Shinyanga Mjini kwa mara tatu kati ya mwaka 1995 na 2000 na mwaka 2005.

Kazi ambazo amewahi kuzifanya serikalini; alikuwa naibu mwanasheria mkuu wa serikali, Naibu Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) mwaka 1966 na elimu yake ana shahada ya sheria kutoka Chuo Kikuu Cha Makarere nchini Uganda.

Ni mzaliwa wa Wilaya ya Kishapu, mkoani Shinyanga akitokea kwenye ukoo wa kichifu wa Makani.
Posted in: | Sunday, June 10, 2012
Maelefu wakiwa wamefurika kwenye mkutano wa hadhara wa CCM unaofanyika  jioni hii kwenye Viwanja vya Jangwani, jijini Dar es Salaam. Mkutano huo ni wa kuwapongeza viongozi wa mashina na matawi waliochaguliwa katika uchaguzi wa CCM ulifanyika kwa ngazi hizo mkoani Dar es Salaam.
Posted in: | Saturday, June 9, 2012
HUKU sakata la mirathi ya marehemu Steven Charles Kanumba aliyekuwa gwiji wa filamu Bongo, likiendelea kufukuta chini kwa chini, baba mzazi mzee Charles Kusekwa Kanumba amegawanya mali za mwanaye, Risasi Mchanganyiko linakufunulia.
Mali za marehemu Kanumba zinazotajwa katika mgawo huo ni pamoja na kampuni yake iitwayo Kanumba The Great Film Company na magari.
HABARI KAMILI
Akizungumza na gazeti hili kwa njia ya simu kutoka Shinyanga, mzee Kusekwa (pichani) alisema yeye kama baba wa marehemu ana jukumu la kuwa msimamizi wa mirathi na kugawa mali za mwanaye.
“Tumekaa huku Shinyanga na ndugu wengine, hili suala la mirathi linapaswa kuwa chini yangu kwa sababu mimi ndiye baba. Kimila za kikwetu (Kisukuma), msimamizi wa mirathi huwa ni baba,” alisema mzee Kusekwa.
Akaongoza: “Kutokana na hilo, nimechukua jukumu la kugawa mali za marehemu mwanangu kwa kuzingatia usawa, haki na vigezo muhimu.”
MGAWANYO WENYEWE
Katika mgawo huo, mzee Kusekwa alitaja sehemu za mali za marehemu Kanumba huku akiacha nyingine.
Mali ambazo hakuzitaja na zinajulikana ni pamoja na akaunti za benki, viwanja viwili vilivyopo Mbezi, Msakuzi nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam pamoja na mali nyingine.
Aliwataja mama mzazi wa marehemu, Flora Mtegoa, mdogo wa Kanumba aliyekuwa akifanya naye kazi kwa karibu enzi za uhai wake, Seth Bosco.
Alisema, katika mgawo huo yeye kama baba anastahili kuchukua gari la kifahari alilokuwa akitumia mwanaye wakati wa uhai wake, aina ya Toyota Lexus na Bi. Mtegoa achukue gari ndogo aina ya Toyota GX 110.
“Ile kampuni ya filamu (Kanumba The Great Film Company) watachukua Seth na dada yake,” alisema mzee Kusekwa.
Kwa sasa, wanaosimamia kampuni hiyo iliyopo Sinza, Mori, jirani na Baa ya Meeda jijini Dar es Salaam ni Seth na dada yake aitwaye Bela.
MPANGO WAKWAMA
Wakati hayo yakiendelea, ilielezwa kuwa mzazi huyo alituma wawakilishi wake kutoka Shinyanga hadi jijini Dar kwa lengo la kufungua mirathi.
Habari za ndani kutoka kwa chanzo chetu makini ambacho hakikupenda jina litajwe gazetini, zinasema kwamba wawakilishi hao walifika katika Mahakama ya Mwanzo ya Kinondoni lakini walikwama.
“Hawafanikiwa kufungua mirathi maana hawakuwa na vielelezo vya kutosha. Walitakiwa kuwa na cheti cha kuzaliwa na cha kifo cha Kanumba pamoja na vielelezo vingine ambavyo hawakuwa navyo,” kilisema chanzo hicho na kuongeza:
“Basi baada ya kukwama, hawakuwa na la kufanya zaidi ya kurudi Shinyanga.”
MAMA KANUMBA
Mama wa marehemu Kanumba, Bi. Mtegoa alipoulizwa anachofahamu kuhusu ujio wa wawakilishi wa mzazi mwenzake alisema: “Nilisikia wamekuja, lakini sijapata kuwaona kabisa. Tumesubiri mpaka sasa kuona kama tutaitwa mahakamani lakini hatujaitwa.”
Akaongeza: “Kiukweli sijui nini kimetokea, maana siku chache baada ya arobaini ya mwanangu, tuliweka kikao hapa Dar na mwenzangu (baba Kanumba) alituma watu wawili waliokuja kumuwakilisha.
“Baada ya makubaliano hayo, tuliwekeana sahihi wanandugu wa pande zote mbili na hata baba Kanumba alikubaliana na watoto wake waliokuja kumuwakilisha kuhusu uteuzi huo...sasa haya tena yananishangaza maana hata mahakamani kufungua mirathi bado sijaenda.”
Posted in: |

MSANII anayewika katika filamu za Kibongo, Salma Jabu ‘Nisha’ ambaye hivi karibuni alivishwa pete ya uchumba na Geofrey Kusey kwa ahadi ya ndoa, amejikuta akibubujikwa machozi baada ya ndoa hiyo kupigwa ‘stop’ na wazazi wake.
Kwa mujibu wa chanzo chetu, ndoa hiyo imezuiwa baada ya kuibuka kwa zengwe ambalo wazazi wa Nisha wameshindwa kulielewa.
Zengwe hilo limekuja kufuatia kuibuka kwa mwanamke mmoja aliyejitambulisha kwa jina la Jennifer ambaye alitumia simu ya mkononi kumchimba mkwara Nisha akimtaka aachane na Kusey kwa sababu ni mume wake.
“Jennifer alimpigia simu Nisha, akamwambia aachane na mumewe ingawa ndoa yao ina migogoro lakini bado ipo hai kwa hiyo hawezi kukubali kuibiwa mume kimachomacho,” kilisema chanzo hicho.
Gazeti hili lilimtafuta msanii huyo kwa njia ya simu ambapo alikiri kutokea kwa tafrani hiyo na kusema kwamba baada ya tukio hilo aliwataarifu wazazi wake ambao walikataa asiolewe na mwanaume huyo.
Aidha, Nisha alisema miongoni mwa mambo yaliyopingwa na wazazi wake kuhusu Kusey ni pamoja na kumvisha pete ya uchumba baa kitendo ambacho hawakukiafiki kutokana na msimamo wa imani yao ya Dini ya Kiislam.
Akaongeza kuwa wazazi wake wamemtaka mwanaume huyo kusitisha safari yake ya Raha Leo, Zanzibar kwa ajili ya kupeleka barua ya posa.
Msanii huyo alisema amesikitishwa sana na kitendo cha Kusey kumficha ukweli kwamba ni mume wa mtu na alikuwa hajamaliza matatizo na mkewe.
Posted in: |

AIBU iliyoje? Tofauti na matarajio ya wengi, Jumapili iliyopita ndani ya Mjengo wa Big Brother Africa (BBA) ‘StarGame’ huko Johannesburg, Afrika Kusini, washiriki watatu walioneshwa mlango wa kutokea wakiwemo Julio Batalia, Hilda (Tanzania) na Teclar (Zimbabwe).
Kutolewa kwa Julio na Hilda kuliongeza machungu kwa Wabongo kwani tukio hilo lilipishana kidogo na lile la Timu ya Soka ya Simba nayo kutolewa kwenye michuano ya Kombe la Shirikisho.
Mara baada ya tukio hilo, Watanzania wengi walikuwa na maoni tofauti huku lawama nyingi zikimwagwa kwa waliowateua washiriki hao ambao watu wengi hawakuwajua kwani hawakuwa mastaa.
“Hii ni aibu kubwa. Tungempeleka Wema (Sepetu) tusingepata aibu hii kwa sababu anafahamika sehemu kubwa ya Afrika kwa hiyo wangempigia kura abaki mjengoni.
“Tatizo tumepeleka watu ambao siyo mastaa. Hakuna cha kujadili kwani Wabongo tulijua mapema kuwa hatuwezi kufika mbali,” ilisomeka sehemu ya maoni hayo kwenye Mtandao wa Kijamii wa Facebook.
Hali ilikuwa hivyo hivyo hata katika mitandao mingine ya kijamii kama Twitter na BBM ambapo hoja za wengi ziliegemea kwenye kuwaponda waliotia sahihi Wabongo hao kwenda mjengoni.

ILIKUWAJE?
Alitangulia Julio kuoneshwa mlango wa kutokea na ilipofika zamu ya Hilda ambaye alikuwa kiongozi mjengoni humo wiki iliyopita, alipoambiwa kura hazikutosha hivyo ametolewa, alijikuta akimwaga chozi na kutia huruma lakini akaambiwa kura ndiyo zimemtoa na siyo Biggie.
WABONGO HAWAKUPIGA KURA?
Ilifahamika kuwa siyo kweli kwamba Wabongo hawakupiga kura kwani hata kama wangepiga mamilioni, Julio na Hilda wasingebaki mjengoni.
Utaratibu ni kwamba pamoja na nchi yako kukupigia kura, unatakiwa pia kupigiwa na nchi nyingine tofauti na ilivyokuwa kwa Julio na Hilda hivyo wakaondoshwa ili wakaendelee na mambo mengine ya kujenga taifa.
Posted in: | Wednesday, May 16, 2012


KITENDAWILI cha nani anaiwakilisha Tanzania kwenye kinyang’anyiro cha Big Brother ‘StarGame’ 2012, Jumapili iliyopita kiliteguliwa baada ya kutangazwa majina ya washiriki wawili, ‘mapatna’ Julio na Hilda.
JULIO
Julio Batalia ni Mtanzania, mkazi wa Dar es Salaam, mwenye umri wa miaka 27, akiwa na Shahada ya Uzamili katika mambo ya mahesabu.

Kwa mujibu wa Julio, alifikia hatua ya kuingia kwenye Big Brother StarGame kutokana na aina ya maisha yake na baada ya rafiki yake kipenzi, Hilda kuwa mmoja wa washiriki anayeamini atakuwa bora zaidi.
Julio alisema Hilda ni mrembo mwenye maisha halisi na siyo ya kuigiza hivyo huwa anapenda kuwa karibu naye muda wote.

“Yuko smati, anavutia sana, Afrika nzima itampenda mno,” alisema Julio akimzungumzia Hilda.
HILDA
Hilda ni Mtanzania, mkazi wa Morogoro mwenye umri wa miaka 28 akiwa ni mfanyabiashara mwenye mtoto mmoja wa kiume ambaye alivutiwa na Biggie mwenyewe (kaka mkubwa) kuingia Big Brother StarGame.
“Anaonekana ni mtu mwenye changamoto ndani ya mjengo hivyo nilijisikia furaha sana nilipochaguliwa kuungana naye kwani nataka changamoto zake,” alisema Hilda na kuongeza:
“Julio ni swahiba wangu mkubwa. Ni mtu mchangamfu, mzuri na mwelewa.”
Kwa mujibu wa Hilda, fedha watakazoshinda, yaani dola za Kimarekani 300,000 (takribani Sh. milioni 500) baada ya kukaa mjengoni kwa siku 91, watazitumia kusaidia makundi mbalimbali ya wasiojiweza kwenye jamii.
Washiriki hao wa Bongo, Julio na Hilda na wale wa Zimbabwe, Maneta na Teclar, tayari wamewekwa kwenye mstari mwekundu wa kuoneshwa mlango wa kutokea Jumapili ijayo hivyo kitakachowaokoa ni wapiga kura kupitia mtandao wa Big Brother Africa.
Posted in: | Tuesday, May 15, 2012

USIKU wa kuamkia Mei 7, mwaka huu ulikuwa ni wa kizaazaa kwa mastaa wa filamu baada ya majambazi kuvamia katika pub ya Aunt Ezekeil iliyopo Mwananyamala Gereji, jijini Dar kwa lengo la kutaka kupora mali.
Majambazi hao walivamia pub hiyo mishale ya saa sita za usiku, wakiwa na bastola na kufyatua risasi na kusababisha uharibifu mkubwa.
Kwa mujibu wa mashuhuda wa tukio hilo majambazi hao ambao walikuwa wawili walifika katika pub hiyo wakiwa katika pikipiki huku mikononi wakiwa wameshikilia bastola waliwaamuru watu wote kulala chini na kutoa kile walichokuwa nacho.
“Tulisikia, wote laleni chini ole wake atakayeleta ubishi,” alisimulia mmoja wa mashuhuda wa tukio hilo.
Alisema, walipogundua kuwa watu wote wametii amri yao hiyo ndipo walipoanza kupita meza hadi meza kukusanya simu na kisha kuingia ndani ya pub na kuchukua fedha na vitu mbalimbali.
Kabla ya majambazi hao hajaondoka rafiki mmoja wa Aunt aitwaye Musa anayeshi Sinza, Dar alionekana kama alitaka kukaidi amri hiyo, ndipo jambazi mmoja akafyatua risasi mbili, moja ikampata mkononi na nyingine mgongoni.
Baada ya kuhakikisha kuwa Musa ametulia baada ya kufyatuliwa risasi hizo, majambazi wale wakawasha pikipiki yao na kutokomea kwa mwendo wa kasi.
Kati ya watu waliokuwepo katika tukio hilo ni msanii maarufu wa filamu nchini, Jacob Steven na Msemaji wa Kampuni ya Usambazaji Filamu ya Steps Entertainment, Selles Mapunda.
“Hakika tumeponea kwenye tundu la sindano, tunashukuru Mungu,” alisema Mapunda.
Posted in: |